Maswi Aitaka Wizara na TLS Kushirikiana kwa Maslahi ya Taifa

Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Eliakim Maswi katika kikao kazi kilichowakutanisha Wizara, Baraza la Uongozi la Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) na Kitengo cha Kuzuia Utakatishaji wa Fedha Haramu kwa lengo la kujengeana uwezo wa utekelezaji wa masharti ya Sheria ya Udhibiti wa Fedha Haramu, kikao kilichofanyika tarehe 31 Oktoba, 2024 katika ukumbi wa Wizara Mtumba, jijini Dodoma.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu, kulijenga Taifa la Tanzania kunahitaji ushirikiano baina ya Taasisi mbalimbali na ni jambo lisilokwepeka hivyo ni vyema kukaa kwa pamoja ili kujua majukumu ya kila mmoja katika kutafuta mustakabali wa kuzuia biashara hiyo. Maswi amesema wapo baadhi ya watu wasiowaadilifu ambao wanaweza kushiriki kwa namna moja au nyingine katika utakatishaji fedha jambo ambalo halikubaliki Kisheria.
Kamishna wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU) Bi. Fatma Simba amesema mapambano dhidi ya biashara hiyo ni jambo linalohitaji nguvu ya pamoja kati ya pande zote na madhara ya utakatishaji wa fedha haramu ni ya Kiuchumi, Kijamii, Kisiasa na Kiusalama ambapo huhatarisha Utawala wa Sheria na Usalama.
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Boniface Mwabukusi amesema TLS ni chombo cha Kisheria na Viongozi wake wameapa kuisimamia Katiba na Sheria na hawapo tayari kusimama kama kizingiti cha kuzuia utekelezaji wa jambo ambalo linaleta maslahi mema katika Taifa.