Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

Muswada Marekebisho ya Sheria ya Ndoa Wakamilika – Sagini

Imewekwa: 23 May, 2024
Muswada Marekebisho ya Sheria ya Ndoa Wakamilika – Sagini

Na William Mabusi – WKS Dodoma

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini amesema Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria imekamilisha uandaaji wa muswada wa marekebisho ya Sheria ya Ndoa na kwamba taratibu zinaandaliwa za kuufikisha Bungeni kwa ajili ya kujadiliwa kisha kupitishwa kuwa sheria kamili.

Mhe. Sagini ameyasema hayo Bungeni Jijini Dodoma Mei 22, 2024 alipokuwa anajibu swali la Mhe. Dkt. Ntara Mbunge wa Viti Maalum aliyetaka kujua lini Serikali italeta Muswada wa Sheria ya Ndoa ili iendane sambasamba na vita dhidi ya ndoa za utotoni.

“Wizara imekamilisha uandaaji wa Muswada wa marekebisho ya Sheria ya Ndoa na hivi sasa muswada huo upo katika hatua za ndani za Serikali na mara hatua hizo zitakapokamilika muswada huo utawasilishwa Bungeni kwa utaratibu wa kawaida.” Alisema.

Mhe. Sagini amesema Serikali ilianza maadalizi muswada huo baada ya kukusanya maoni ya Wadau mbalimbali wakiwemo Wazee wa kimila, Viongozi wa kidini, Wanataaluma, Wanafunzi wa ngazi mbalimbali, Watu mashuhuri na  Waheshimiwa Wabunge juu ya maboresho ya sheria hiyo kuhusu kuondoa mabishano ya umri upi kwa sasa uwe wa kuoa au kuolewa.