Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

Rais Mwinyi afunga Mkutano wa Mawaziri wa Sheria wa Nchi za Madola

Imewekwa: 08 Mar, 2024
Rais Mwinyi afunga Mkutano wa Mawaziri wa Sheria wa Nchi za Madola

Na William Mabusi WKS – Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amefunga Mkutano wa Mawaziri wa Sheria wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Madola na kuzitaka nchi wanachama kutumia teknolojia na kuhakikisha haki inawafikia wote bila kuyasahau makundi maalum.

Mkutano huo wa Siku tano uliokuwa unafanyika Visiwani Zanzibar ukiongozwa na Mwenyekiti Waziri wa Katiba na Sheria wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana, umefungwa rasmi leo tarehe 08 Machi, 2024.

“Nchi wanachama tujitahidi kuhakikisha haki inaendelea kutolewa kwa wote na sasa kwa kuwa nchi wanachama umeazimia kujikita katika kutumia teknolojia haki iwafikie makundi maalum wakiwemo walemavu. Amesema Dkt. Mwinyi huku akisisitiza umuhimu wa matumizi ya namna nyingine ya mawasiliano yakiwemo matumizi ya alama kwa watu wenye changamoto ya usikivu.

Akisoma taarifa ya mkutano huo kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana, Waziri wa Sheria na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Rwanda Mhe. Dkt. Emmanuel Ugirashebuta amesema “Mawaziri wa Sheria wamepokea na kujadili maudhui yanayohusiana na teknolojia na uvumbuzi ili kuongeza ufanisi, kupunguza gharama za kuendesha mashtaka na kurahisisha mchakato wa kisheria katika upatikanaji wa haki. Umoja ni nguvu, tutaendelea kushirikiana katika maeneo yote tuliyokubaliana katika majadiliano wakati wa mkutano.”

Akiongea kwenye mkutano ulioandaliwa wa Wanahabari Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola MH. Patricia Scotland KC ametoa shukrani zake za dhati kwa nchi ya Tanzania na Zanzibar kwa kuuratibu vyema mkutano huo ambao lengo lake ni kudumisha umoja miongoni mwa nchi wanachana.

“Mkutano huu umekuwa ni wenye mafanikio makubwa, tunaelewa miongoni mwa nchi wanachama zimo nchi ambazo zimepiga hatua kimaendeleo, zipo ambazo zinaendelea, kuna nchi kubwa na ndogo hivyo tutumie kile tulichonacho kuwanufaisha wanachama wengine” alisema na kuagiza uzingatiaji wa utoaji wa haki kwa kuyafikia maeneo ya pembezoni akiitaja kampeni ya Mama Samia ambayo sasa imeshika kasi kote Tanzania Bara na Zanzibar kama mfano.