Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

Serikali Itaendelea Kuimarisha Michezo – Dkt Biteko

Imewekwa: 06 Oct, 2023
Serikali Itaendelea Kuimarisha Michezo – Dkt Biteko

Na George Mwakyembe – WKS Iringa

Naibu Waziri Mkuu Mhe. Dkt. Dotto Biteko amesema Serikali itaendelea kuimarisha michezo kwa watumishi wote nchini ili kujenga mahusiano mazuri baina yao lakini pia kuimarisha afya.

Mhe. Biteko ameyasema hayo alipokuwa akizindua michezo ya SHIMIWI inayofanyika Mkoani Iringa tarehe 04 Oktoba 2023. Michezo hii ambayo inajumuisha watumishi wa Wizara, Idara pamoja na Taasisi mbambali za umma imeanza tangu tarehe 29 Septemba, 2023 kwa michezo ya mpira wa miguu, mpira wa mikono pamoja na kuvuta kamba.

Mhe. Biteko amesema “Michezo hii ya SHIMIWI ni ya watumishi wa Serikali, tusiruhusu iharibiwe kwa kuingiza mamluki ambao siyo watumishi. Serikali imeleta hii michezo ili watumishi muweze kuimarisha afya lakini pia kuleta hari mpya mahala pa kazi,”

Aidha, Dkt. Bitteko amewaasa Makatibu wote wa Wizara pamoja na Wakurugenzi wa Taasisi pamoja na Idara kusimamia kikamilifu michezo mahala pa kazi na kuwaruhusu watumishi kushiriki kwenye michezo mbalimbali kwa kuwajengea mazingira mazuri ya ushindani.

Naye Mwenyekiti wa SHIMIWI Taifa Bw. Daniel Mwalusamba amefafanua kuwa  michezo hii ni ya 37 na  imejumuisha  jumla ya watumishi 2,765  ambao wanatoka kwenye  Wizara 24,  Taasisi  za Serikali 14 pamoja na Wakala wa Serikali 5 wote wamejisajili katika michezo mbalimbali ikiwemo kuvuta kama na kukimbia.

Bw. Mwalusamba amewashukuru Makatibu Wakuu wote pamoja na Wakuu wa Taasisi za Umma kwa kuwaruhusu watumishi kushiriki michezo ya SHIMIWI na kuamini kuwa mwaka ujao watawaruhusu watumishi wengi zaidi.