Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

Serikali Kuendelea na Utaratibu wa Plea Bargaining – Sagini

Imewekwa: 23 May, 2024
Serikali Kuendelea na Utaratibu wa Plea Bargaining – Sagini

Na William Mabusi – WKS Dodoma

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini amesema utaratibu wa kisheria wa Plea - Bargaining katika mashauri ya jinai umekuwa na faida nyingi na hivyo Serikali itaendelea kuutumia.

Mhe. Sagini ameyasema hayo Bungeni Jijini Dodoma Mei 22, 2024 alipokuwa anajibu swali la Mhe. Abubakar Damian Asenga (Kilombero) aliyetaka kujua kama Serikali inaona bado kuna umuhimu wa Sheria ya Plea - Bargaining.

”Tangu kuanza kwa utaratibu huu mwaka 2019 hadi Juni 2023 jumla ya mashauri 423 yamemalizika kwa utaratibu  Plea Bargaining ambayo yalihusisha watuhumiwa 1,040.  Kiasi cha Shilingi 54,643,730,080.13 zilirudishwa Serikalini kupitia utaratibu huu na shilingi 2,083,384,927.70 zilirudishwa kwa wahanga wa uhalifu. Kutokana na faida hizo, Serikali bado inaona umuhimu wa kuwa na utaratibu huu wa kisheria katika mashauri ya jinai.” Alisema.

Utaratibu wa kisheria wa Plea – Bargaining ulianza kutumika baada ya Serikali kufanya marekebisho ya Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai Sura ya 20 kwa kuongeza vifungu vya 194A, 194B, na 194C kwa kuanzisha utaratibu wa kukiri makosa kwa makubaliano maalum kati  ya mshtakiwa na Serikali ukiwa na lengo la kupunguza muda wa upelelezi na usikilizwaji wa mashauri; kupunguza mlundikano wa mahabusi; kuwezesha kubaini namna uhalifu unavyotendeka; pamoja na kubaini mitandao ya kiuhalifu.