UKATILI KINARA MIGOGORO INAYOHITAJI MSAADA WA KISHERIA-WAZIRI MKUU

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa amesema ukatili na unyanyasaji wa kijinsia ni miongoni mwa migogoro inayosumbua jamii kwa kiwango kikubwa huku wananchi wakichelea kutoa taarifa za vitendo vya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia.
Mhe. Majaliwa ameyasema hayo leo Juni 16 2025 Katika uwanja wa Maturubai Mbagala jijini Dar es Salaam wakati akizindua Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia huku akitoa rai kwa wananchi wote, watoto, wanaume na wanawake wanaopatia vitendo hivyo kutoa taarifa hususan katika kampeni hii ili wasaidiwe.
"Ukatili umegawanyika katika maeneo mengi, nieleze machache tu, la kwanza ni ukatili wa kimwili. Ukatili wa kimwili ni kitendo cha kudhamiria kufanya vurugu na kutumia nguvu ili kumsababishia mtu madhara ya kimwili au mateso na haya yapo mengi," amefafanua Mhe. Majaliwa.
Ameongeza kuwa, "kupigwa kupita kiasi, wengine wanachomwa moto, Kubaka mtu na ipo tabia ya watu wanashika nywele za mtu anamtikisa tikisa, huo ni ukatili pia. Kwahiyo yametokea hayo myalete hapa kwenye kampeni ndiyo mahali pa kusaidiwa na kujua namna nzuri ya kukabiliana nayo".
Mhe. Majaliwa amesema kuna ukatili ambao umekuwa ukipigwa vita muda wote ambao ni ukatili wa kingono yaani kumlazimisha mtu kushiriki shughuli za kingono bila ridhaa, ubakaji, ulawiti, kubusu mtu akiwa hataki, wanawake pia wanapitia tatizo la kushikwashikwa mwili bila ridhaa yake.