Watetezi wa Haki za Binadamu Zingatieni Sheria - KM Maswi

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Ndg. Eliakim Maswi ametoa wito kwa mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) kuhakikisha wanafuata sheria za nchi, taratibu zilizowekwa, na kufanya kazi kwa ushirikiano bila ubinafsi.
Maswi ametoa wito huo Machi 18, 2025 jijini Dodoma, wakati akifunga mafunzo ya siku mbili kwa wanachama wapya wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC.)
Amesema kuwa mashirika hayo yana nafasi ya kutoa maoni na mapendekezo juu ya sheria zinazowasimamia, ili serikali iweze kufanya mabadiliko pale inapohitajika kwa ajili ya kuimarisha haki za binadamu kwa wananchi.
Aidha, amewataka wanachama wapya wa THRDC kuwa mabalozi wa haki za binadamu katika maeneo wanayotoka, kwa kuhakikisha wanachochea mabadiliko chanya kwenye jamii zao.
Kwa upande wake, Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, amesema kuwa ukiukwaji wa haki za watoto umekuwa changamoto kubwa inayozidi kukithiri nchini jambo ambalo wanapaswa kuongeza nguvu katika kukabiliana nalo.