Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

Chana Asema Serikali Inathamini Uhai wa Kila Mtu

Imewekwa: 10 Oct, 2023
Chana Asema Serikali Inathamini Uhai wa Kila Mtu

Na Lusajo Mwakabuku – WKS

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana amesema adhabu ya kifo kwa nchi yetu imekuwa ya lazima pale tu inapohusisha kuondoa uhai wa binadamu mwingine kwani hata katika kosa la uhaini pamoja na kuwa inatoa adhabu ya kifo, bado inatoa nafasi kwa Jaji kuamua vinginevyo isipokuwa pale ambapo kutakuwa kumetokea mauaji ndio adhabu hiyo itakuwa lazima.

Waziri Chana ameyasema hayo alipokuwa akihutubia katika hafla ya Maadhimisho ya Kimataifa ya Kupinga Adhabu ya Kifo Duniani yaliyoandaliwa na TLS leo tarehe 10 Oktoba, 2023 Jijini Dar es salaam.

Waziri Chana akaongeza kuwa katika utekelezaji wa sheria nchini mwetu, Tanzania kama Taifa inathamini haki ya kuishi na imejipambanua kulinda haki hiyo na ndiyo maana imeweka katika Katiba yake Ibara ya 12 kuwa kuna haki ya kuishi na inatambua itifaki na mikataba mingi ya kimataifa inayoongelea haki ya kuishi.

Aidha, Waziri Chana akaongeza kuwa pamoja na kuwa adhabu ya kifo ipo kwa mujibu wa Sheria,  Lakini Serikali bado inathamini na kulinda uhai wa kila mtanzania na ndiyo maana hata wale waliopewa adhabu ya kifo wakiumwa wanatibiwa kwa gharama ya Serikali.

Maadhimisho ya Kimataifa ya Kupinga Adhabu ya Kifo Duniani huadhimishwa tarehe 10 ya mwezi Oktoba kila mwaka ikiwa na lengo la kuhamasisha kufutwa kwa adhabu ya kifo katika nchi zinazotekeleza adhabu hiyo.