ELIMU YA SHERIA NI MSINGI WA AMANI, MAENDELEO NA MSHIKAMANO - DKT. NDUMBARO

Waziri wa Katiba na Sheria ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Songea Mjini, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema Elimu ya masuala ya kisheria ni msingi wa amani, maendeleo endelevu na mshikamano katika jamii.
Dkt. Ndumbaro amesema hayo wakati akiendelea kutoa elimu kwa wananchi wa Manispaa ya Songea kuhusu masuala ya utawala bora na namna ya kutatua migogoro kwa njia ya kisheria.
Mafunzo hayo yamefanyika katika kata zote 21 za Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa viongozi wa Serikali kuhakikisha wananchi wanapata elimu ya haki na msaada wa kisheria.
Akizungumza na wananchi, Dkt. Ndumbaro ameeleza kuwa viongozi katika ngazi mbalimbali wanapaswa kupata mafunzo ya kisheria ili waweze kushughulikia kwa ufanisi changamoto mbalimbali za kijamii na kuimarisha misingi ya utawala bora.
Katika hatua nyingine, Mhe. Dkt.Ndumbaro amepongeza juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita kupitia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwa kuendeleza sekta ya michezo nchini.
Amesema michezo si tu burudani, bali ni chanzo cha ajira, uchumi, afya bora, na kukuza amani katika taifa.
Amehimiza wananchi kuunga mkono juhudi za Serikali na kushirikiana na viongozi wao katika kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Kuhusu maendeleo ya miundombinu na uchumi, Dkt. Ndumbaro ametangaza mpango wa kuwasilisha serikalini ajenda ya ujenzi wa chuo kikuu kipya, pamoja na viwanda na maghala ya kuhifadhia mazao ndani ya Jimbo la Songea Mjini.
Ameeleza kuwa uwekezaji huo utachochea thamani ya mazao ya wakulima, kuongeza fursa za ajira kwa vijana na kuinua uchumi wa eneo hilo kwa ujumla.
Amewaomba wananchi kushikamana na viongozi wao ili kufanikisha ndoto ya Songea mpya yenye maendeleo jumuishi.