Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

Kamati Yaipongeza Serikali Ujenzi wa Jengo la Wakili Mkuu wa Serikali

Imewekwa: 27 Mar, 2024
Kamati Yaipongeza Serikali Ujenzi wa Jengo la Wakili Mkuu wa Serikali

Na William Mabusi – WKS Dodoma

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Florent Kyombo ameipongeza Serikali kwa juhudi inazofanya za kuendelea kukamilisha majengo ya kudumu ya Wizara na Taasisi za Serikali kwenye eneo la Mji wa Serikali Mtumba, Jijini Dodoma.

Mhe. Kyombo amesema hayo wakati Kamati hiyo ilipotembelea ujenzi wa Jengo la kudumu la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ambalo ujenzi wake umefikia asilimia 49, tarehe 27 Machi, 2024 eneo la Mtumba kunakojengwa Mji wa Serikali.

“Tunaipongeza Serikali kwa kuendelea kutenga bajeti ya kujenga majengo makubwa kama hili la Wakili Mkuu wa Serikali, kiu yetu ni kuona jengo hili linakamilika na kuanza kutumika kama ilivyokusudiwa. Hivyo tuiombe Serikali kuongeza kasi ya malipo kwa Mkandarasi na Msimamizi wa mradi kuwawezesha kufanya kazi ili mradi huu ikamilike kwa muda uliopangwa.” Alisema.

Katika ukaguzi huo Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo aliyemwakilisha Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana, amesema Wizara itaendelea kufanya kazi kwa kusaidiana na kumshauri Mshitili ambaye ni Wakili Mkuu wa Serikali katika kukabiliana na changamoto zozote kwenye ujenzi huo.

Awali akitoa taarifa ya ujenzi, Mkandarasi wa mradi huo Eng. Baraka Mosha amesema ujenzi unaendelea vizuri pamoja na kuwepo changamoto kadhaa ikiwemo kuchelewa kwa malipo.

Akijibu baadhi ya hoja, Kaimu Naibu Wakili Mkuu wa Serikali Bw. Mark Mulwambo amesema ofisi yake imeingia makubaliano na Mkandarasi kutumia mpango wa Manunuzi wa Milestone, mpango ambao utawezesha upatikanaji wa pesa kabla ya kazi kufanyika, badala ya mpango wa Mkandarasi kulipwa kwa Certificate baada ya kufanya kazi.