Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

''KAMPENI YA MSAADA WA KISHERIA YA MAMA SAMIA NI MKOMBOZI WA WANANCHI WA KONDOA''-NYANGASA

Imewekwa: 07 May, 2026
''KAMPENI YA MSAADA WA KISHERIA YA MAMA SAMIA NI MKOMBOZI WA WANANCHI WA KONDOA''-NYANGASA

Mkuu wa  Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma Mhe. Fatma Almas Nyangasa amesema maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuanzisha Kampeni ya  Msaada wa Kisheria  nchi nzima, imekuwa mkombozi kwa wananchi hasa wa pembezoni mwa nchi ambao hawana kipato cha kuweza kuzifuata huduma za Mahakama, kugharamia Mawakili  pamoja na kuwapa maarifa  wananchi ambao hawana uelewa  juu ya masuala ya  kisheria.

Mhe. Nyangasa amebainisha hayo leo Jumanne  Mei 05, 2026 wakati akizungumza na  Wananchi katika Uwanja wa Ubembeni Kata ya Kondoa Mjini, kuhusu ujio wa Kampeni hiyo ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia katika Wilaya ya Kondoa.

Amebainisha kuwa katika utendaji wa kila siku wa  Ofisi yake changamoto kuu ni wananchi kutokuwa  na uelewa wa kisheria, suala ambalo Kampeni hiyo itakwenda kuitatua kwa kiasi kikubwa.

"Ukienda kwa wananchi unagundua kuwa asilimia kubwa ya changamoto tulizonazo ni  kwasababu wananchi kutojua wapi kwa kuanzia kwahiyo elimu hii inayotolewa katika Kampeni hii ni kitu cha muhimu na cha msingi sana kwa Watanzania na nikiri kuwa Mhe. Rais Samia aliona mbali  katika hili  kwasababu  kama  hujui  taratibu ni ngumu sana kufikia kwenye utatuzi wa changamoto yako kwa haraka. 

Niwahakikishie hii fursa ni muhimu sana kwetu wananchi wa Kondoa, naomba tuitumie vizuri" Amesema Mhe. Nyangasa.

Kwa upande Wakili wa Serikali kupitia Wizara ya katiba na Sheria na mratibu wa kampeni hiyo Wilaya ya Kondoa Everitt Magile Steph ameeleza kuwa changamoto kubwa waliyoikuta kwa wananchi wa Wilaya hiyo inasababishwa na  migogoro ya ardhi.

Ametoa rai pia kwa wananchi wa Wilaya hiyo wenye changamoto mbalimbali za kisheria kufika kwenye vituo vya kutolea huduma ili kuweza kuhudumiwa  mpaka kufikia tarehe Mei 15, 2026, zoezi hili litakapokamilika.