Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

"KUIMARIKA KWA SEKTA YA SHERIA UKANDA WA AFRIKA MASHARIKI-CHACHU YA UPATIKANAJI HAKI"

Imewekwa: 23 Feb, 2026
"KUIMARIKA KWA SEKTA YA SHERIA UKANDA WA AFRIKA MASHARIKI-CHACHU YA UPATIKANAJI HAKI"

Ushirikiano wa  kikanda kupitia  vyama vya kitaaluma  katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya Sheria vinaonesha dhamira ya dhati ya wanachama wake kubadilisha  uzoefu,kujenga uwezo na kuwa na viwango bora vya utoaji huduma kwa wanachama wake katika kuwahudumia  wananchi.

Kwa mantiki hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na  Sheria Ndg. Eliakim Maswi  leo tarehe 20, Februari 2026, Mtumba jijini Dodoma, amekutana na kufanya mazungumzo na  Uongozi wa Chama cha Mawakili wa  Afrika Mashariki ukiongozwa na Katibu wa Chama  hicho Wakili John Seka. 

  Mazungumzo hayo yameonesha  dhamira ya dhati  ya kuimarisha sekta ya Sheria katika ukanda wa Afrika Mashariki mkazo  ukiwa  katika utoaji wa elimu ya kisheria kwa umma na msaada  wa kisheria kwa wananchi wasiojiweza. 

Katika mazungumzo hayo, Pande zote mbili zimejadili namna bora ya kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali katika utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala (ADR) na katika kufanya majadiliano ya mikataba ili kuimarisha usimamizi wa rasilimali za umma  na kulinda maslahi ya Taifa. 

Katika hatua nyingine  Uongozi wa  Chama hicho umeishukuru Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria kwa kufanikisha upatikanaji wa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Makao Makuu ya Chama hicho ambacho kwa sasa kina jumla ya Mawakili elfu 45,000 . 

Hatua hiyo inaonesha kukua kwa taaluma ya Sheria na fursa za ushirikiano wa kikanda jambo ambalo linatarajia  kuleta manufaa makubwa kwa jamii, ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa upatikanaji wa huduma za kisheria,kupunguza migogoro kupitia utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala.

Ikumbukwe kuwa Wizara ya Katiba na Sheria hivi karibuni imeingia makubaliano na  taasisi mbalimbali katika utoaji wa huduma za kisheria ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wote na huduma za kisheria zinaboreshwa kwa ustawi wa wananchi.