MAGEUZI YA WIZARA YA KATIBA NA SHERIA NA TAASISI ZAKE YAIKOSHA KAMATI YA BUNGE
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ikiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Edwin Enosy Swalle imeridhia na kuipitisha Randama ya Mpango na Bajeti kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ya Wizara ya Katiba na Sheria na taasisi zake katika kikao kilichofanyika leo tarehe 28 Machi, 2026 Bungeni jijini, Dodoma.
Randama hiyo imesheheni vipaumbele vilivyojikita katika kuimarisha sekta ya Sheria kwa kufanya mageuzi ya kiutendaji na uwajibikaji kwa kuifanya kuwa mhimili mkuu wa maendeleo ya Taifa kufikia Dira 2050.
Wajumbe wa Kamati katika nyakati tofauti tofauti wameipongeza Wizara na Taasisi zake kwa jitihada za kiubunifu zinazofanyika katika kuimarisha huduma za upatikanaji wa haki kwa Watanzania kupitia Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia , na programu ya "Sema na Waziri" ambapo wananchi wanaweza kupata huduma za kisheria kwa kupiga simu katika kituo cha huduma kwa mteja cha wizara bila malipo.
Kuwasilishwa na kuidhinishwa kwa Randama hiyo ni hatua muhimu kuanza kwa maandalizi ya mwisho ya Hotuba ya Bajeti itakayowasilishwa rasmi katika Mkutano wa Bunge la Bajeti la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linalotarajiwa kuanza karibuni.