Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

MSLAC Imesaidia Kukuza Uelewa wa Kisheria na Haki za Binadamu kwa Wananchi na Watendaji

Imewekwa: 23 Feb, 2025
MSLAC Imesaidia Kukuza Uelewa wa Kisheria na Haki za Binadamu kwa Wananchi na Watendaji

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Abdalah Sagini amesema Kampeni ya Kitaifa ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia imesaidia kukuza uelewa wa kisheria na haki za binadamu kwa wananchi na watendaji wa serikali huku pia ikikuza na kuimarisha huduma za ushauri wa kisheria na unasihi kwa waathirika wa vitendo mbalimbali ya kikatili.

Mhe. Sagini amebainisha hayo Februari 19, 2025 wakati wa uzinduzi wa Kampeni hiyo Mkoani Lindi, akisema pia kampeni hiyo imesaidia kukuza imani kwa wananchi katika utatuzi wa migogoro mbalimbali kwa njia mbadala sambamba na kukuza uelewa wa watendaji wa serikali ngazi ya jamii kuhusu masuala mbalimbali yahusuyo sheria, utawala bora na utawala wa sheria kama nguzo kuu ya maendeleo, amani na utulivu wa nchi.

Naibu Waziri Sagini pia amesema Kampeni hiyo kufikia Januari mwaka huu ilikuwa imezinduliwa kwenye mikoa 17 na Februari hii inazinduliwa na kutekelezwa kwenye mikoa mitano na mpango wa serikali ni kwamba kufikia mwezi Mei 2025, kampeni hiyo iwe imekwisha tekelezwa kwenye mikoa yote ya Tanzania bara na Tanzania visiwani, akisisitiza kuwa Wizara ya Katiba na Sheria itaendelea kutoa mafunzo mbalimbali kwa watendaji wa serikali katika kuhakikisha kuwa dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassan inafikiwa katika kuhakikisha haki inapatikana kwa kila anayestahili.