Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

"MSLAC Itusaidie. Kuna Migogoro Imetushinda" – DC Kissa

Imewekwa: 30 May, 2024
"MSLAC Itusaidie. Kuna Migogoro Imetushinda" – DC Kissa

Hyasinta Kissima – WKS Njombe

Mkuu wa Wilaya ya Njombe Mhe. Kissa Kasongwa amesema kuwa kupitia Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia katika Wilaya ya Njombe ipo migogoro ya muda  mrefu ambayo imekuwa ikijadiliwa na kuhamishiwa kwa Viongozi mbalimbali lakini ufumbuzi wa migogoro hiyo umekuwa haupatikani.

Mhe. Kissa aliyasema hayo Mei 29, 2024 wakati akiwasilisha salamu za Serikali katika Mkutano wa Baraza la Waheshimiwa Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Njombe uliofanyika katika ukumbi wa makao makuu ya Halmashauri yaliyopo Kijiji cha Kidegembye  Kata ya Lupembe Wilayani Njombe.

"Tunaupongeza uongozi wa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye chini ya uratibu wa Wizara ya Katiba na Sheria waliamu kuja na ubunifu wa kuleta huduma za Kisheria za bure Mama Samia Legal Aid Campaign. Kuna mifupa huko imetushinda Waheshimiwa Madiwani. Zipo kesi za miaka mingi sana Wananchi wanahamisha malalamiko kwa Viongozi mbalimbali kila anapokuja Kiongozi mpya kesi zinaanza upya na muafaka haufikiwi. Mama Samia Legal Aid ipo Wilayani kwetu na leo hii tutaanza na mgogoro wa Lupembe Saccos ambao naamini huu mfupa hautatushinda."Alisema Kissa.

Mheshimiwa Kissa amesema kuwa, mgogoro wa Lupembe Saccos ni kero ambayo inawaumiza Wananchi wengi na wengi wanaona wanapoteza haki yao kutokana na Wanachama wa Saccos hiyo kuwekeza mamilioni ya fedha kwa kipindi kirefu na kwa sasa wanapokwenda kuomba fedha zao Saccos hiyo haina fedha za kuwapatia wanachama wake.

Kwa upande wake Wakili wa Serikali Mkuu kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Candid Nasua amesema kuwa, kupitia Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia timu ya Wataalamu wakiwemo Wanasheria na Mawakili ipo kwa ajili ya kuhakikisha kila mgogoro unasikilizwa na kupatiwa ufumbuzi ili haki iweze kutendeka kwa kila anayestahili.

Dhumuni la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha kuwa kila mwanachi mwenye nacho na asiyekuwa nacho mwenye uhitaji wa huduma za kisheria anasaidiwa  na anapata haki yake bila gharama yoyote.