Serikali Yatoa Msimamo Kuhusu Dhana ya Watu Asilia (Indigenous People)

Na Lusajo Mwakabuku - WKS Geneva
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Hazara Chana, amefanya mazungumzo na Mtaalam Maalum wa Umoja wa Mataifa anayeangalia masuala ya Haki za Watu Asilia (Indigenous People) Bwana Francisco Cali Tzay tarehe 3 Julai 2024.
Kupitia kikao hicho, Waziri wa Katiba na Sheria, Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hapa Geneva Mhe. Balozi Dkt. Abdallah Possi na Katibu Mkuu wa Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo wameeleza msimamo wa Serikali kutounga mkono dhana ya watu asilia kwa kuzingatia mazingira ya Tanzania.
Aidha, wamefafanua mafanikio ya kisera, kisheria na kitaasisi ya kuhakikisha kila mtanzania anapata haki zake za msingi bila kubaguliwa. Vilevile, walieleza jinsi suala la Ngorongoro linavyoshughulikiwa kwa uwazi na kwa haki kwa kuwa wakazi katika hifadhi ya Ngorongoro wanahama kwa hiari.
Waziri Chana alitumia nafasi hiyo kumuahidi mtaalam huyo ushirikiano kipindi atakapo kuja nchini kujionea mwenyewe hali halisi ya jinsi suala hili linavyotekelezwa.
Kikao hiki ni sehemu ya majadiliano yanayotokana na ushiriki wa Tanzania katika Kikao cha 56 cha Baraza la Haki za Binadamu kinachoendelea jijini Geneva - Switzerland katika ofisi za Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.