Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

TANZANIA YAJIVUNIA  MIAKA 20 YA MAHAKAMA YA AFRIKA

Imewekwa: 03 Mar, 2026
TANZANIA YAJIVUNIA  MIAKA 20 YA MAHAKAMA YA AFRIKA

Tanzania imeendelea  kujivunia  kuwa mwenyeji  wa  Mahakama  ya  Afrika ya  Haki za Binadamu na Watu, hali inayoashiria imani kubwa kwa Tanzania
katika masuala ya  amani, utulivu na kuheshimu misingi ya haki barani Afrika. 

Akizungumza leo tarehe 2 Februari, 2026  mbele ya Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Dramani Mahama, wakati  wa ufunguzi wa mwaka wa Mahakama kwa niaba ya Waziri wa Katiba na  Sheria, Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Zainab  Katimba amesema Tanzania inajivunia kuwa nchi mwenyeji wa Mahakama hiyo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2006 kwamba imekuwa  mshirika thabiti katika kuimarisha mfumo wa haki za binadamu wa Afrika. 

Ameeleza kuwa licha ya mafanikio yaliyopatika kupitia  Mahakama hiyo ikiwa ni pamoja na  kuendelea  kusimamia maono ya “Suluhisho za Kiafrika kwa Changamoto za Kiafrika”, katika kipindi cha miaka 20 ya Mahakama hiyo bado imeendelea kukumbwa na changamoto kadha wa kadha zikiwemo baadhi ya nchi kutoidhinisha mamlaka yake au kujitoa kwenye tamko la Ibara ya 34(6) ya Itifaki yake. 

Naibu Waziri  Katimba alibainisha kuwa Tanzania imechukua hatua za kutekeleza baadhi ya maamuzi ya Mahakama hiyo katika mifumo ya ndani ya utoaji haki, ikiwemo maboresho ya sheria na maamuzi ya mahakama za ndani yanayozingatia misingi iliyowekwa na Mahakama ya Afrika.