WIZARA YAWANOA MAWAKILI NA MAAFISA SHERIA KUHUSU UTATUZI WA MIGOGORO KWA NJIA MBADALA
Wizara ya Katiba na Sheria imetoa mafunzo kwa Mawakili na Maafisa Sheria wa Serikali kutoka Sekretarieti za Mikoa kwa lengo la kuwajengea uwezo kuhusu mbinu za utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala(ADR), ili kuongeza ufanisi katika kushughulikia upatikanaji wa haki kwa wakati na kupunguza mlundikano wa kesi mahakamani kwa kushughulikia migogoro nje ya Mahakama.
Akifungua rasmi mafunzo ya Mawakili na Maafisa Sheria wa Serikali tarehe 16 Machi, 2026 Kibaha mkoani Pwani, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa Pwani Dkt. Kusirye Ukio akimuwakilisha Katibu Tawala mkoa wa Pwani Bi. Pili Mnyema amesema ni muhimu sasa Mawakili na Maafisa Sheria wa Serikali kuongeza nguvu katika kutatua migogoro ya wananchi kwa njia mbadala ili kurahisisha upatikanaji wa haki kwa wananchi, kuondoa uhasama na kujenga mahusiano mazuri katika jamii.
"Ni muhimu watalaam hawa wakisheria kuendelea kujifunza na kujengewa uwezo kuweza kukabiliana na changamoto kwa weledi na kwa ufanisi katika kuhudumia watanzania" amesema Ukio.
Aidha, Ukio amesisitiza kuwa ulimwengu sasa umejikita katika kutatua changamoto mbalimbali katika jamii kwa njia Mbadala kwa muda mfupi na kwa gharama nafuu kitu ambacho kimewanufaisha watanzania walio wengi wasioweza kukidhi gharama za huduma.