Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

KUTOA MAONI KUHUSU UBORESHAJI WA MFUMO WA SHERIA NCHINI NA ELIMU YA UANASHERIA KWA VITENDO

01 Feb, 2023


T A N G A Z O K W A U M M A


Kufuatia taarifa ya matokeo ya wanafunzi wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo ya hivi karibuni, na baada ya kuibuka kwa taharuki miongoni mwa wanajamii wakiwemo wanazuoni na wadau mbalimbali wa sekta ya sheria kuhusu ufaulu mdogo wa wanafunzi katika tasnia ya Sheria, tarehe 12 Oktoba, 2022 Mheshimiwa Dkt. Damas D. Ndumbaro (Mb.), Waziri wa Katiba na Sheria aliunda Kamati Maalum ya kufanya tathmini ya mfumo wa elimu ya Sheria nchini na changamoto zinazoukabili mfumo huo ikiwa ni pamoja na namna mafunzo ya uanasheria kwa vitendo yanavyotolewa.
Pamoja na mambo mengine, Kamati hiyo imepewa jukumu la kushauri namna ya kuboresha mfumo huo ili kukidhi mahitaji ya taaluma ya Sheria kwa lengo la kuwa na ushindani wa kitaifa na kimataifa. Kamati katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Hadidu za Rejea ilizopewa, itapokea maoni kwa maandishi pia kuwasikiliza wadau mbalimbali ana kwa ana.
Kwa kuwa siyo wananchi wote watapata fursa ya kufika mbele ya Kamati kutoa maoni, Mhe. Dkt. Harrison G. Mwakyembe, Mwenyekiti wa Kamati anawaalika wananchi na wadau wenye mapenzi mema na uboreshaji wa mfumo wa elimu ya sheria nchini na elimu ya uanasheria kwa vitendo, kuwasilisha maoni kwa maandishi ili kuiwezesha Kamati kupata maoni mengi kadri inavyowezekana na hatimaye kushauri ipasavyo. Mwisho wa kupokea maoni ya maandishi ni tarehe 24 Oktoba, 2022 saa 10:00 jioni.
Maoni hayo yawasilishwe kupitia barua pepe ya km@sheria.go.tz, mitandao ya kijamii ya twitter: @Sheria_Katiba; Instagram @katibanasheria_ au                                                                                              WhatsApp kwa namba 0742 910529.


IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
WIZARA YA KATIBA NA SHERIA
18 Oktoba, 2022