Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

SERIKALI YACHUKUA HATUA MADHUBUTI KUHAHAKISHA HAKI ZA WANAWAKE NA WASICHANA

Imewekwa: 18 Mar, 2026
SERIKALI YACHUKUA HATUA MADHUBUTI KUHAHAKISHA HAKI ZA WANAWAKE NA WASICHANA

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Katiba na Sheria imewasilisha juhudi mbalimbali  zinazolenga kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wanawake na wasichana, katika Mkutano wa 70 wa  Kamisheni ya Hali ya Wanawake Duniani unaoendelea katika Jiji la New York, nchini Marekani.

Akizungumza katika mkutano wa pembezoni uliofanyika machi 16, 2026 jijini humo, Mkurugenzi Msaidizi wa  Sehemu ya Uratibu wa  Msaada wa Kisheria, Bi. Lucy Diganyeck ameeleza kuwa serikali imechukua hatua madhubuti katika kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata haki zao kwa urahisi.

Alitaja baadhi ya jitihada hizo kuwa ni pamoja na utekelezaji wa  Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia ambapo kupitia kampeni hiyo Takriban wanawake 2,135,902 walifikiwa na walipatiwa huduma za msaada wa kisheria. 

Katika hatua nyingine Diganyeck ameeleza jitihada za matumizi ya teknolojia katika kutoa huduma za kisheria kwa wanawake ambapo kupitia kituo cha huduma kwa mteja cha Wizara kimewezesha kutoa msaada wa haraka kupitia simu, hususan kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yenye changamoto za kijiografia na miundombinu.

Mkutano huo unaendelea ukiwa na kaulimbiu isemayo: “Kuimarisha Upatikanaji wa Haki kwa Wanawake na Wasichana Wote: Mchango wa Huduma za  Msaada wa Kisheria katika Kukabiliana na Ukatili wa  Kijinsia na Kufikia Uwezeshaji wa Wanawake Wote.”