Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

Kamati Yapokea na Kuridhia Makadirio ya Bajeti 2024/25

Imewekwa: 25 Mar, 2024
Kamati Yapokea na Kuridhia Makadirio ya Bajeti 2024/25

Na William Mabusi – WKS Dodoma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imepokea na kuridhia Mpango wa Makadirio ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa fedha 2024/25 huku ikiahidi kuitetea kwenye Bunge lijalo la Bajeti.

Makadirio ya bajeti hiyo yamewasilishwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana tarehe 25 Machi, 2024 kwenye Ofisi za Bunge Dodoma. Katika kikao hicho Dkt. Chana aliambatana na Katibu Mkuu Bi. Mary Makondo, Naibu Katibu Mkuu Dkt. Khatibu Kazungu pamoja na Wakuu wote wa Taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo.

Akichangia baada ya kuwasilishwa kwa makadirio hayo, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Florent Kyombo amesema, ”kwetu sisi kupokea makadirio haya ya bajeti siyo kwamba tumemaliza kazi bali kazi ndiyo kwanza tumeianza kuhakikisha kwamba yale tuliyokubaliana tunayasimamia na kuyatetea kadri itakavyowezekana ili yapitishwe kwenye vikao vingine na yatekelezwe.”

Naye Mhe. Edward Olelekaita Kisau ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati hiyo ameipongeza Wizara kwa utekelezaji wa majukumu yake kadri ya ushauri wa Kamati huku akitoa wito kwa Serikali kuwapa ushirikiano wa kutosha na kuendelea kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali kuwaongezea ufanisi katika kutekeleza majukumu yao.

”Tunaona Mawakili wa Serikali wanashinda kesi nyingi na zenye pesa nyingi za ndani na hata za Kimataifa na kuokoa kiasi kikubwa cha pesa, tunataka kuona Mawakili hao wakipewa ushirikiano mkubwa, tuone Mawakili hawa walau wanapewe barua za ”recognition” tusiseme tu uzalendo, uzalendo peke yake haitoshi. Mawakili binafsi wakipelekewa kazi kabla ya kuchaji wanaangalia kiasi cha pesa watakachookoa halafu ndiyo wanachaji gharama za kesi.”

Aidha, Kamati hiyo imeshauri Serikali kuendeleza miradi ambayo imeshaanza kutekelezwa na tayari wananchi wanafurahia utekelezaji wake hata kama Washirika wa Maendeleo wataonesha kutoendelea kufadhili miradi hiyo kwenye bajeti ijayo. Walitaja Mradi kama usajili wa watoto chini ya umri wa miaka mitano na Mama Samia Legal Aid Campaign miongoni mwa miradi mingine.

Akitoa salaam katika kikao hicho Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo amesema Wizara na Taasisi zake itaendelea kutekeleza majukumu sawa na matarajio ya wananchi.

“Tutaendelea kufuata maelekezo ya Kamati katika kutekeleza majukumu ya sekta ya sheria ili wananchi wapate matarajio makubwa ambayo wanayo kutoka Wizarani na Taasisi zinazosimamia haki. Tunaendelea kupokea maelekezo yenu na ahadi yetu ni kwamba tutaenda kuyatekeleza ili kufikia malengo ya bajeti. Aidha, katika kuziba pengo la bajeti inayokadiriwa, Wizara itaendelea kubuni miradi ya maendeleo kwa kushirikiana na Wadau wa Ndani na Nje na tayari mawasiliano kati yetu na Wadau yameanza. Amesema Bi. Makondo.