Waziri wa Katiba na Sheria nchini Tanzania Dkt. Damas Ndumbaro ameeleza kuwa Wizara yake inaendelea na uratibu na utekelezaji wa Kampeni ya Kitaifa ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia, ambapo kufikia sasa Tayari kampeni hiyo imetekelezwa kwenye mikoa 25 ya Tanzania bara, Dar Es salaam ikisalia peke yake kwa bara.
Akiwasilisha hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na sheria kwa mwaka 2025/26 leo Jumatano Aprili 30, 2025 Bungeni Dodoma, Waziri Ndumbaro ameliambia Bunge kuwa kufikia Mwezi Juni Mwaka huu, kampeni hiyo itaanza rasmi kwa Mkoa wa Dar Es salaam ili kuhitimisha rasmi mikoa yote ya Bara.
"Tangu kuanza kwa kampeni hii tarehe 27, mwezi wa nne mwaka 2023 kampeni hii tayari imefanyika kwenye mikoa ya Dodoma, Manyara, Shinyanga, Ruvuma, Simiyu, Singida, Iringa, Mara. Songwe, Morogoro, Njombe, Katavi, Tabora, Geita, Kigoma, Mtwara, Mwanza, Kilimanjaro, Mbeya, Lindi, Rukwa, Pwani, Arusha, Tanga na Kagera." Ameongeza Waziri Ndumbaro.
Katika hatua nyingine, Waziri Ndumbaro amezungumza pia kuhusu utekelezaji wa kampeni hiyo Visiwani Zanzibar, akieleza kuwa kampeni hiyo tayari imetekelezwa kwenye mikoa ya Kaskazini Pemba, Mjini Magharibi na Kaskazini Unguja na kwasasa inatekelezwa mwenye mikoa ya Kusini Pemba na Kusini Unguja, ikitarajiwa kukamilika Mwezi Mei mwaka huu.