Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

HOMERA: HAKUNA TAIFA IMARA BILA SHERIA IMARA

Imewekwa: 01 Sep, 2026
HOMERA: HAKUNA TAIFA IMARA BILA SHERIA IMARA

Makamishna wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, wametakiwa kutumia uzoefu na maarifa waliyonayo kuhakikisha Taifa linakuwa na sheria   bora zitakazosaidia katika kutekeleza Dira 2050.

Hayo yamewekwa bayana na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera wakati akifungua mafunzo elekezi kwa Makamishna wapya wa ofisi ya Tume  ya Kurekebisha Sheria  Tanzania yaliyofanyika  leo 01 Septemba, 2026, jijini Dodoma

Dkt. Homera amesema serikali  imekua ikikutana na changamoto ya utekelezaji wa sheria ambazo hazijafanyiwa utafiti, jambo linalopelekea kuwa na sheria zilizopitwa na wakati na kuzitaka wizara na taasisi kabla ya kutunga au kubadili sheria kushirikiana na Tume kabla ya kuwasilisha mapendekezo kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali au Mwandishi Mkuu wa Sheria.

Waziri  Homera amesema hakuna Taifa  imara bila kuwa na sheria imara na zenye tija kwa Taifa, na amewapongeza Makamishna waliomaliza muda wao  na kuwataka Makamishna wapya kumsaidia Mhe. Rais katika kuhakikisha Sheria za Nchi zinaendana na wakati hasa katika kutekeleza Dira 2050.

Awali, akimkaribisha Mhe. Waziri, Mwenyekiti wa Tume hiyo, Mhe. Jaji Winfrida  Korosso, amesema Tume imejipanga vyema kutekeleza maelekezo ya  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuishukuru Wizara kwa ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya  Tume, hatua iliyowezesha ufanisi wake.

Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania imeundwa chini ya kifungu cha 3 cha Sheria ya Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania sura 171 na majukumu yake yameainishwa katika kifungu cha 4 cha sheria hiyo ikiwa na lengo la kuhakikisha nchi inakuwa na sheria himilivu na zinazoakisi mazingira ya Tanzania.