Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Katiba na Sheria

MAAFISA WA SERIKALI WAJENGEWA UWEZO KUHUSU MIKATABA NA SHERIA ZA KIMATAIFA

Imewekwa: 10 Jul, 2026
MAAFISA WA SERIKALI WAJENGEWA UWEZO KUHUSU MIKATABA NA SHERIA ZA KIMATAIFA

Kituo cha Ufanisi wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu (African Court Coalition – ACC) kwa kushirikiana na wataalam kutoka Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu na  Chama cha Wanasheria wa Afrika Mashariki (EALS) wameendesha kikao cha kuwajengea uwezo maafisa mbalimbali wa Serikali. Mafunzo hayo yamejikita katika  majukumu ya Mahakama ya Afrika, sheria  na mikataba ya kimataifa na kikanda.

Akifungua mafunzo hayo, Mratibu wa ACC, Sophia Ebby, alisema warsha hiyo imelenga   kuimarisha uelewa wa pamoja kuhusu Mahakama ya Afrika na wajibu wa wadau mbalimbali.

"Tunatarajia kuwa majadiliano yatakayofanyika yataimarisha ushirikiano katika kuendeleza haki, utawala wa sheria na ulinzi wa haki za binadamu," alisema Bi. Ebby.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Haki za Binadamu Wizara ya Katiba na Sheria, Bi. Nkasori Sarakikya, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa  Serikali kuimarisha upatikanaji haki kwa kuwajengea uwezo maafisa husika kwenye mnyororo wa haki.

Aliwahimiza washiriki kushiriki kikamilifu, akisisitiza kuwa Serikali inategemea utaalamu wao katika kutekeleza wajibu wake wa kukuza na kulinda haki za binadamu.